6/13/18

KADHIA YA ONGEZEKO LA JOTO

Utangulizi
Kumekuwa na matukio mbali mbali yanayotokea mahali mbali mbali duniani kama kiashirio cha mabadiliko ya hali ya hewa katika uso wa dunia, ikiwemo vimbunga, mafuriko, ukame, kuongezeka kwa kina cha maji baharini, upotevu wa jamii za mimea na wanyama na kuyeyuka kwa barafu katika mzingo wa Aktiki ulio kaskazini mwa dunia. Haya ni baadhi tu ya matukio ambayo ni viashiria, kwamba inatupasa kucukua hatua za makusudi kukabili hali hii.

MADA
Kwa huku upande wa kaskazini mwa dunia, kumekuwa na malalamiko ya ukosefu wa theluji katika msimu mwafaka. Kwa kawaida, kwa tropiki ya Kansa msimu wa baridi huanza mwezi Novemba. Wenyeji wa huku huwa wanapenda sana kuteleza katika theluji na imezoeleka kila mara kwamba kila ifikapo mwezi Desemba basi kila mahali huwa na theluji ya kutosha kwa sababu joto huwa chini ya nyuzi sifuri, na kila mtu hufurahia hali hii. Lakini kwa miaka ya hivi karibuni kumekuwa na mabadiliko yasiyo ya kawaida katika hali hii, kwamba kwa sasa inatokea kwamba ifikapo Desemba kunakuwa hakuna theluji kabisa na joto linakwa liko juu ya nyuzi sifuri. Kwa maana hiyo, msimu wa baridi umekuwa mfupi sana ikilinganishwa na miaka ya nyuma. Wenyeji wanasema kuwa mabadiliko haya hasi yameanza hasa kuonekana kuanzia mwaka 1986 na kuendelea, na hali inazidi kuwa mbaya kadri miaka inavyozidi.
Kwa upande wa tropiki ya Kaprikoni, chini ya Ikweta, huku ndio huwa na ukame uliokithiri, kutokana na mabadiliko haya. Ikumbukwe kwamba mnamo mwaka 2005 kulikuwa na ukame ambao uliathiri sana upatikanaji wa maji, kiasi cha kusababisha matatizo katika uzalishaji wa umeme. Kwa mujibu wa baadhi ya tafiti za kitaalamu, hali hii huenda ikawa ni matukio ya kawaida iwapo nchi zinazoongoza kwa uchafuzi wa hali ya hewa hazitafanya juhudi za makusudi katika kupunguza hewa ya kaboni dayoksaidi itokayo katika viwanda vyao.
Inapaswa kila mtu ajivike majukumu ya kukabiliana na hali hii kwa kufanya yafuatayo.

1. Utunzaji wa Nishati
Kuzima vifaa vya umeme kama vile taa, pasi, runinga, majiko na feni ama viyoyozi iwapo kwa muda huo vinakuwa havihitajiki. Hii husaidia kupunguza matumizi ya nishati yasiyo ya lazima, hivyo kupunguza pia uzalishaji wa nishati husika.

2. Kutumia Usafiri wa Jumuiya
Iwapo kunakuwa hakuna ulazima wa kutumia usafiri binafsi, basi ni vyema kama tutatumia usafiri wa jumuiya kama vile mabasi, treni na meli kwa safari zetu mbali mbali. Kitendo hiki kitapunguza kiwango cha nishati kitumikacho na mitambo hii. Kitendo hiki kiende sambamba na matumizi ya baiskeli kwa safari fupi fupi ambazo hazimlazimu mtu kutumia gari ama pikipiki.

3. Utunzaji wa Maji
Tutumie maji tuliyonayo kwa kujibana. Hii itasaidia sana kupunguza matumizi yake, kiasi kwamba yale machache tuliyo nayo yanaweza kabisa kututosha. Pia ni vyema kama tutakuwa na utaratibu wa kusafisha maji yaliyokwisha kutumika, ili yatumike tena kwa matumizi mengine kama vile umwagiliaji wa mashamba na ujenzi.

Inawezekana, tutimize wajibu wetu.

No comments: