1/17/23

Mbinu mojawapo ya kumaliza upungu wa umeme nchini


Mnamo tarehe 1 na 2 Novemba 2022 kulikuwa na kongamano la Nishati Safi ya kupikia, lililofanyika mkoani Dar es Salaam, kama lilivyorusha kwenye vyombo mbalimbali vya habari Tanzania na nje ya Tanzania. Kwenye hilo kongamano wadau waliongelea kupika kwa kutumia umeme. Walisema ni njia rahisi na ya haraka kwa kuwa kwa sasa kuna vifaa vya kisasa vya kupikia kwa umeme na vina ufanisi mkubwa. Wengi walikuwa na wasiwasi na huu mgao unaoendelea sasa nchini, kwamba unaweza kuweka chakula chako jikoni halafu umeme ukakatika na ukashinda njaa. Wachangia mada wengine walisema kupika kwa umeme sio kwamba tu ni ghali, ila umeme hautoshelezi (ni wa mgao).
Kuhusu upungufu wa umeme, nina ushauri ufuatao ambao unatufaa sana kwa muda mfupi ujao. Mbinu mojawapo ambayo inaweza kutusaidia kuzalisha umeme ni kuzalisha umeme na joto kwa wakati mmoja (Combined Heat and Power) kwa kutumia takataka tunazozalisha mitaani. Kila wilaya na kila mkoa una dampo/jaa la takataka. Kwenye haya madampo inawezekana kuweka mitambo ya kuchoma taka (baada ya kuzichambua na kuzitenganisha) na kuzalisha mvuke ambao unaendesha mifuo ya umeme. Teknolojia hii si ngeni na kwa hapa Tanzania inatumika Mkoani Njombe (Tanwat) na TPC mkoani Kilimanjaro. Tanwat wanatumia masalia ya miti baada ya kuvunamiti ya nguzo, badala ya taka, TPC wanatumia masalia ya miwa badala ya taka za mtaani. Iwapo mitambo hii tungeiweka kila mkoa (inawezekana iwapo tutaipa kipaumbele), tusingekuwa na upungufu wa umeme tunaolalamikia kila leo. Kutegemea umeme wa maji kwa enzi hizi si wazo endelevu hata kidogo, kutokana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamesababisha kukauka kwa mito mingi na hivyo kuathiri sana uzalishaji wa umeme. Wazo jingine lenye uwezekano ni kutumia umeme wa jua na upepo. Kampuni ya Rift Valley Energy tayari wamefunga mitambo ya kuzalisha umeme wa upepo wilayani Mufindi mkoani Iringa. Inawezekana pia kuzalisha umeme mahali pengine penye upepo.
 
Pichani (nyuma yangu) ni mtambo wa kuzalisha umeme kwa kutumia takataka zilizochambuliwa. Unamilikiwa na Manispaa ya Mji wa Karlstad, Sweden.