6/13/18

MABADILIKO YA HALI YA TABIANCHI

UTANGULIZIMnamo tarehe 18 Septemba 2007, nilihudhuria semina kuhusu mabadiliko hasi ya tabianchi na madhara yake katika viumbehai na katika maisha ya mwanadamu kwa upekee. Semina hii ilifanyika katika jiji la Oslo, Norway na ilishirikisha wadau wa taaluma mbali mbali kama vile wanasosholojia, wahandisi, wasanifu, wanasiasa, wataalamu wa ardhi na maji na wataalamu wa mazingira, kwa kutaja wachache, kutoka mabara yote. Hakika ilikuwa ni semina nzuri sana, kwani kulikuwa na mijadala mikali sana hasa kuhusu namna ya kuyakabili masuala haya kwa undani na kwa mbinu zinazokubalika katika mazingira ya sasa. Tulipata wasaa wa kuangalia picha za video zilizopigwa nchini Kenya, Nepal, Norway na Uganda, na wahusika toka nchi hizi ndio walikuwa wazungumzaji wakuu kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, kadri walivyoshuhudia toka katika nchi zao.


MADAMtoa mada Joseph Kones kutoka Kenya aliwasilisha ushuhuda wake wa mabadiliko ya hali ya hewa kutoka mahali alipozaliwa, eneo la Maasai Mara, lililo katika bonde la mto Mara. Ikumbukwe kuwa bonde hili limesambaa mpaka Tanzania, katika mbuga ya wanyama ya Serengeti. Akasema kwamba kati ya miaka ya hamsini na sabini kulikuwa na mvua za kutosha na zilikuja kwa msimu maalum. Kwamba, mvua za masika zilikuwa inanyesha kuanzia mwezi Machi hadi Mei na ndio msimu ambao wakulima walipanda mazao yao. Lakini kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa ya hivi karibuni, hali imekuwa sio hiyo tena, kwani kwa sasa mvua za masika hazina msimu maalum kwa eneo hilo, ambalo kwa sasa linakabiliwa na ukame wa mara kwa mara. Pia mvua zinazonyesha katika eneo hilo kwa sasa hazina kiwango maalum kama zamani, kwamba zinaweza kuja nyingi na kusababisha mafuriko, ama zikaja chache na kutotosheleza mahitaji ya mimea, ama zisije kabisa katika msimu husika kiasi cha kusababisha ukame. Hali kadhalika, mtoa mada aliongelea suala la mbu waletao malaria, kwamba katika kipindi tajwa hapo juu kulikuwa hakuna mbu wa malaria katika eneo hilo, lakini kuanzia mwishoni mwa miaka ya themanini kumekuwa na malaria katika eneo hilo. Kutokana na ukame wa mara kwa mara, kumekuwa na baa la njaa ambalo husbabishwa na mazao kukauka kabla ya kukomaa, mifugo inakufa kutokana na kukosa malisho na kukauka kwa vyanzo vya maji kwa ujumla. Hali kadhalika, kumekuwa na ugomvi wa mara kwa mara kati ya jamii za wafugaji wa Kipsigi na Wamasai, kugombea malisho na maeneo ya kunyweshea mifugo yao. Kumekuwa pia na magonjwa yanayosambaa kwa njia ya maji, kama vile kichocho na homa za matumbo. Kumekuwa na uchafuzi wa mito na vyanzo vya maji, kutokana na wingi wa mifugo usioendana na uwezo wa vyanzo hivi kukidhi idadi hii ya mifugo. Akatoa wito kwa jumuiya za kimataifa pamoja na wadau wengine, kuangalia namna ya kuyaokoa maeneo haya kutokana na athari hizi.

Naye mtoa mada Frank Turyatunga (mwakilishi wa UNEP) kutoka nchini Uganda alikuwa na yake ya kusimulia kutoka nchini mwake. Alisema kwamba kuna mto unaotenganisha nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Uganda. Mto huu enzi za miaka ya sitini na sabini ulikuwa hauathiriwi sana na mafuriko ya mara kwa mara, lakini kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa kwa sasa mto huo hufurika mara kwa mara na unamomonyoa kingo zake na kusababisha eneo kubwa la ardhi ya kumegwa na kusombwa na maji, na wakati mwingine mto huhama na kumega eneo la Uganda. Hali hii inasababisha Uganda kupoteza ardhi yake, kwani mto huu ni mpaka kati ya nchi hizi mbili, kwa maana hiyo kama mto unahama na kuelekea upande mwingine basi nchi nyingine hufaidi sehemu ya ardhi ambayo imehamwa na mto. Ikumbukwe kuwa eneo hili pa limegunduliwa kuwa na utajiri wa mafuta, kwa hiyo inaweza kuwa chanzo cha migogoro hapo baadaye. (Zingatia kuwa mto Songwe ulio kati ya nchi za Malawi na Tanzania una tabia ya namna hii, ya kuhama mkondo mara kwa mara kiasi cha kusababisha matatizo katika eno husika)

Mtoa mada Norbu Sherpa kutoka Nepal alikuwa na yake ya kuzungumza, hasa kutokana na athari za mafuriko ya mara kwa mara kutokana myeyuko wa barafu kutoka katika kilele cha milima ya Himalaya, unaochangiwa na ongezeko la joto duniani. Huyu alitoa ulinganifu wa athari kwa kufuata miaka, kama nilivyotaja hapo juu. Kwa ujumla mtoa mada huyu alilalamikia suala la kumegwa kwa ardhi kando ya kingo za mito, kiasi cha kuwalazimu wao kuhama maeneo hayo na kuelekea maeneo ambayo yana mwinuko zaidi, ili kujiepusha na athari za mafuriko hapo baadaye. Aliongelea suala la kusombwa kwa mazao, makazi na kupotea kwa maisha ya watu kutokana na mafuriko.

MJADALAShuhuda zilizojadiliwa hapo juu ndio zimekuwa kilio cha nchi nyingi duniani na athari hizi hata nchini mwetu zinaonekana waziwazi. Vimbunga vya mara kwa mara (1995), mafuriko (kumbuka el nino 1997/1998), ongezeko la magonjwa, ukame wa mara kwa mara (1993/1994) , (2005/2006) na ongezeko la joto ni baadhi tu ya athari za mabadiliko tajwa ya hali hewa. Ukiachilia ushuhuda wa uzoefu kutoka kwa wazee wetu na wakaazi wa maeneo mbali mbali, kuna mbinu za kisayansi za kupima mabadiliko haya hasi ya hali ya hewa na athari zake. Mbinu hizi zipo nyingi sana, ila nitagusia chache tu kwa ufupi. Mbinu hizi ni kama zifuatazo.

Ongezeko la JotoOngezeko la joto (mean annual temperature) hupimwa kwa kutumia vipimajoto vya satelaiti pamoja na vile vilivyo ardhini katika vituo vya hali ya hewa na kufanyiwa ulinganifu wa kitaalamu (modelling) kutoka wakati mmoja na mwingine ama kutoka mwaka mmoja na mwingine. Mfano, vipimo vya vilivyochukuliwa miaka ya arobaini hadi miaka ya sitini hulinganishwa na vile vinavyochukuliwa sasa na kukokotoa tofauti yake. Mara nyingi athari za ongezeko hili la joto ni pamoja na kuongezeka kwa myeyuko wa barafu ambapo husababisha mafuriko, kusambaa kwa magonjwa kama vile malaria na kukauka kwa vyanzo vya maji. Si ajabu basi tukisikia kuwa maeneo kama Kitulo, Makete, Mufindi ama Marangu hayakuwa na mbu waletao malaria katika miaka ya sitini na sabini lakini sasa kuna malaria!

Kupungua kwa kasi ama Kupotea kwa jamii za MimeaKuna baadhi ya mimea ambayo huwa inaathirika sana kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa. Upotevu huu hupimwa kulingana na wakati na kufanyiwa ulinganifu. Kwamba kwa mfano, kama mwaka 1930 kulikuwa na mimea 20 ya aina fulani katika meta moja ya eneo, na kwa sasa kuna mimea 8 ya jamii hiyo katika eneo hilo hilo la meta moja ya eneo, basi tunaweza kujua kwamba upotevu wa mimea ni kiasi gani kwa kufanya ulinganifu sasa, tangu eneo hilo lilipowekwa kumbukumbu ya mimea hiyo. Kwa sababu mimea na wanyama hushirikiana katika ikolojia na mfumo lishe, athari kwa mimea pia huleta athari kwa wanyama. Iwapo mimea mingi inakuwa imeondolewa katika eneo fulani , maji hayawezi kutunzwa ardhini, kwani mimea husaidia kutunza maji kwa kuzuia mionzi ya jua kutua moja kwa moja ardhini. Zingatia kwamba eneo tajwa linalofayiwa utafiti niliotaja hapo juu ni lile ambalo halijaathiriwa na shughuli za moja kwa moja za binadamu kama kilimo, ukataji miti na upandikizaji wa mimea mipya.

Mtawanyiko wa MajiKila eneo la ardhi duniani lina mtawanyiko wake maalum wa maji (surface run-off) kwa kila kilometa ya eneo. Kadri athari za kimazingira zinavyoongezeka ndio mtawanyiko huu hupungua ama kuongezeka. Kwa ufafanuzi ni kwamba, joto likichanganyikana na upepo huongeza kasi ya upumuaji (evaporation) ya mito na maziwa, hivyo kupunguza uwingi wa maji. Iwapo ongezeko hili ni la kudumu, basi na upungufu huu huwa ni wa muda mrefu. Hali kadhalika kwa maeneo yenye barafu, iwapo kutakuwa na ongezeko la joto, basi myeyuko wa barafu huwa ni wa kiwango cha juu na huenda ukawa ni wa kudumu hivyo kuongeza uwingi wa maji wa eneo husika, hasa wakati wa joto. Vipimo vya maji vya eneo husika ndivyo hufanyiwa ulinganifu kutokana na wakati na kutathmini athari zake.

Kutokana na athari hizi basi, kumekuwa na mwamko katika maeneo mbali mbali hapa duniani kuhusu namna bora ya kukabili athari za uharibifu wa mazingira na ongezeko la joto.
Tufanye nini basi ili kukabiliana na athari hizi? Nini kifanyike ili vyanzo vya maji visikauke? Tufanye nini ili mvua zije kwa wakati na za kutosha? Jadili.

No comments: