6/5/06

SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI...TUNAJIFUNZA NINI?

Kila mwaka, tarehe tano Juni ni siku ya mazingira duniani. Watu katika nchi mbali mbali hapa ulimwenguni huadhimisha siku hii kwa namna mbali mbali, wengi aghalabu hufanya shughuli mbali mbali za utunzaji wa mazingira. Kwa hapa kwetu nchini, sherehe hizi huambatana na kufanya kazi za utunzaji mazingira, kama vile uokotaji wa taka mahali mbali mbali, upandaji wa miti sehemu za wazi na kadhalika. Lakini kwa upande mwingine, hapa nchini kwetu upandaji wa ,miti kitaifa hufanyika kila mwaka siku ya Januari mosi, yaani siku ya mwaka mpya. Nadhani hii tarehe imewekwa makusudi kwa sababu kwa maeneo mengi (kama si yote) hapa nchini huwa ni msimu wa mvua. Kwa hio, ili miti iliyopandwa iote vizuri, ni lazima ipate maji ya kutosha, kutokana na mvua hizi.

Ni kwa nini basi tunaadhimisha siku hii?
Nitaanza kwa kufafanua maana ya dhana hii ya "mazingira" . Mazingira, kwa ujumla wake, ni vitu vyote ambavyo humzunguka mwanadamu. Vitu hivi ni kama maji, miti, milima, mabonde, miamba na kadhalika. Tunaadhimisha siku hii kwa sababu nyingi. Sababu kubwa ni kwamba, bila mazingira, mwanadamu hawezi kuishi. Kwa hiyo mwanadamu hana budi kuboresha mazingira yake ili aendelee kuishi. Mwanadamu akiharibu mazingira, basi anaharibu uhai wake mwenyewe.
Kila mwaka kunakuwa na semina na makongamano sehemu anuwai hapa duniani, kwa ajili ya kujadili suala hili la mazingira kwa mapana yake, lengo kubwa ikiwa ni kuyaboresha. Mmoja wa mikutano hii maarufu ni ule uliofanyika katika mji wa Kyoto nchini Japan tarehe 11 Desemba mwaka 1997. Mkutano huu ulitengeneza mkataba wa kupunguza uchafuzi wa mazingirana ulianza kufanya kazi tarehe 16 Februari 2005, ambapo ulilenga kupunguza ongezeko la joto duniani, ambao ulifikia maamuzi magumu ya kupunguza uharibifu wa anga kwa kupunguza gesi zenye sumu kutoka viwandani. Mpango (mkataba) huu hufanya kazi kupitia chombo kijulikanacho kama "United Nations Framework Convention on Climate Change" (UNFCCC). Kumbuka kuwa Marekani haikutia sahihi mkataba huu, kwa kuogopa kuua viwanda vyake, ambavyo huzalisha gesi nyingi sana za sumu duniani. Chombo hiki ndicho hutoa mwongozo wa kiwango cha gesi za sumu zinazotakiwa kutolewa kutoka viwandani ili kutoharibu "ozone" ambayo ni kiwambo cha gesi ambacho huzuia mionzi ya jua yenye madhara kutufikia moja kwa moja toka angani. Mpaka sasa, nchi 163 zimeweka sahihi katika mkataba huu.
Mkutano huu wa Kyoto ulitanguliwa na ule wa tarehe 5 Juni mwaka 1992 katika mji wa Rio de Janeiro nchini Brazil, ambao nao malengo yake yalikuwa ni kupunguza uharibifu wa mazingira na kutunza bio anuwai.

Hali ya mazingira ikoje hapa kwetu?
Hali ya mazingira yetu kwa ujumla ni mbaya, kwamba tunashindwa kuyatunza kwa kwa usahihi. Ni suala la kawaida kwa watu mbali mbali kulima na kujenga katika vyanzo vya maji, mbuga za wanyama na hifadhi za taifa. Ni kawaida kwa wenye viwanda kumwaga taka zenye sumu katika mito na vijito, na mifano hai ipo mingi tu. Ni kawaida kutupa ovyo chupa za maji tukishakunywa maji, na ni kawaida kujisaidia haja ndogo mahali palipoandikwa "USIKOJOE HAPA". Ni kawaida kwa watu kutupa taka chini pamoja na kwamba mahali hapo pameandikwa 'TUPA TAKA HAPA". Kwa nini? Kwa faida ya nani?Hatumkomoi mtu, ila ni sisi wenyewe tunajisababishia vifo vinavyoweza kuepukika kabisa. Tunapotiririsha maji ya sumu ya viwandani katika mito, ilhali tunavua samaki katika mito hiyo hiyo tunatarajia nini? Tunakatazwa kutumia zebaki katika kusafishia madini lakini hatuachi, kwa nini? Tunaharibu vyanzo vya maji na mito inakauka, tunakosa maji na umeme, hatuoni kuwa tunajinyima haki? Kwa nini? Ni viwanda vingapi vinachafua hali ya hewa kwa gesi za sumu? Hatuvifahamu viwanda hivi? Tumechukua hatua gani?
Je tunachukua hatua madhubuti katika utunzaji na uhifadhi wa mazingira?
Jadili
Soma makala maalum ya siku ya mazingira hapa

No comments: