1/5/07

MAISHA MBADALA

UTANGULIZI
U hali gani msomaji wa blogu yangu. Kwa leo nakuletea mambo mawili muhimu, hasa kuhusu suala zima la mazingira. Katika mapumziko ya Krismasi na mwaka mpya, nilifanikiwa kuzulu jiji la Copenhagen wao wanaita Kobenhavn, nchini Denmark, na kwa kweli nilifurahi sana.

MADA
MIFUO YA UMEME WA NGUVU YA UPEPO

Katika ufukwe wa bahari kwanza kabisa nilipokewa na msururu wa mifuo ya umeme inayoendeshwa kwa nguvu ya upepo, kwa kweli inaonyesha ni kwa jinsi gani hawa wenzetu wanajali suala la kupunguza ongezeko la joto duniani. Mifuo hii ni mingi sana nchini humu, na kuna watu wanadai kuwa inawezekana kabisa kuwa nchi hii ndiyo inayoongoza kwa kuwa na mifuo mingi ya umeme huu wa nguvu ya upepo.
Mitambo hii wao wameiweka katika ufukwe kwa sababu maalum, kwamba kandoni mwa bahari kuna upepo wenye nguvu sana kutokana na mawimbi ya bahari, kwa hiyo wakaona ni bora watumie nguvu hiyo katika kuzalisha umeme. Kwa upande wa kwetu sisi, bado tupo nyuma ya wakati kuhusu suala zima la kutumia nguvu ya upepo kuzalisha umeme. Tuna ufukwe mrefu sana katika bahari ya Hindi kuanzia Mtwara hadi Tanga, lakini bado hatujafanya matumizi sahihi ya ufukwe huu. Pia tuna maziwa makubwa matatu, nayo ni Tanganyika, Nyasa na Viktoria, ambapo pia ingewezekana kutumia fukwe zake kuzalisha umeme wa nguvu ya upepo, lakini hali si kama hivyo. Mpaka sasa bado sijajua kwa yakini sababu zinazotufanya tushindwe kutumia nguvu hii ya upepo kuzalisha umeme.

ADHA ZA MIFUO HII
Pamoja na hatua hii nzuri ya kuweka mifuo ya umeme, kumezuka malalamiko kutoka kwa baadhi ya wanamazingira. Malalamiko haya yanadai kuwa mifuo hii ya umeme huwa inaharibu mandhari asilia ya eneo husika, kwa maana ya kwamba iwapo mifuo hii itawekwa mahali basi sura ya mahali hapo inabadilika, kwa sababu mifuo hii ni mikubwa sana. Kuna mifuo mingine huwa na kimo cha hadi kufikia meta mia moja kwenda hewani na huchukua eneo kubwa sana, kwa hiyo wanamazingira hawa hawajapendezwa kwa kiasi fulani na suala hili. Sababu ya pili ni kwamba, katika maeneo haya na mengineyo ambayo yana mifuo hii huwa kunakuwa na viumbe hai wengine kama ndege ambao huishi katika maeneao hayo, kwa hiyo basi ndege ambao huruka karibu na maeneo haya hupata ajali kwa kugongana na pangaboi za mifuo hii inapozunguka, hasa kunapokuwa na ukungu ama giza wakati wa mchana. Na kama nilivyodokeza hapo juu, mifuo mingi ipo katika fukwe za bahari na kama tunavyojua kuwa katika bahari na pembezoni mwake kuna ndege wavuvi kama batamaji, heroe, furukombe wavuvi, bundi wavuvi na kadhalika, basi ndege hawa wavuvi ndio ninaoongelea katika makala hii, kuwa wanagongana na pangaboi za mifuo hii.
Kwa hiyo pamoja na kwamba tunapata faida ya umeme kupitia mifuo hii, kuna hiyo tahadhari ambayo huwa tunapaswa kuizingatia, hasa tunapokuwa tunapanga mipango endelevu ya kuweka mifuo ya namna hii.

BAISKELI
Suala lingine ambalo ningependa kuliongelea kwa leo ni uwingi wa baiskeli katika jiji la Copenhagen. Kuna baiskeli nyingi sana hapa mahali hadi zinakuwa kero kwa wakati fulani. Kwa upande mwingine, uwingi huu unamaanisha kuwa kiasi kikubwa cha watu huwa wanatumia baiskeli katika safari fupi fupi za mjini hapa. Niliwahi kuliongelea suala hili katika makala zangu zilizopita, kuwa njia moja wapo ya kupunguza msongamano wa vyombo vya moto katika majiji makubwa kama hili ni kutumia usafiri wa kupunguza baiskeli kwa safari ambazo hazilazimu kutumia gari. Suala hili la kutumia baiskeli pia linasaidia kupunguza hewa zenye sumu kutokana na moshi magari. Inawezekana basi ikawa ni mkakati wa serikali katika kupunguza msongamano wa vyombo vya usafiri, kwamba wakasisitiza kutumia baiskeli kwa kiwango kikubwa kama ilivyo mahali hapa.




TUFANYE NINI?
Kwa kutumia mifano hii miwili inatakiwa tutoke na mtazamo mpya kuhusu suala zima la mazingira, kwa sababu kwa namna moja ama nyingine tusipojitahidi kuzuia ongezeko la joto duniani kuna hatari ya kupoteza asilimia kubwa ya viumbe wetu wa asili. Si suala geni kwa kusikia kwa walio wengi sababu kwa sasa tunasoma katika maandiko mbali mbali ya kumbukumbu za kihistoria kuwa hapo zamani kulikuwa na wanyama wanaitwa Dinosaurs na walitokomea kabisa katika uso wa dunia, kutokana na sababu anuwai, kwa hiyo na sisi kama hatutafanya juhudi za kuzuia hali hii basi kuna hatari kubwa sisi pamoja na viumbe wanaotuzunguka kutokomea kabisa katika uso huu wa dunia. Pamoja na kwamba kuna nguvu za asili kama matetemeko ya ardhi na volkano ambavyo huweza kubadili sura ya nchi na uoto wa asili, si vibaya kama nasi tutachukua hatua katika kudhibiti kile ambacho kipo ndani ya uwezo wetu kwa wakati huu. Mambo haya ni pamoja na kupunguza kiwango cha hewa chafu za viwandani, kupunguza kemikali katika maji ambayo huwa tunayamwaga katika bahari zetu, kupunguza kama si kuzuia kabisa utupaji ovyo wa masalia ya nishati nyuklia na la muhimi zaidi ni kupunguza matumizi ya madawa ya kilimo yenye sumu.
Inawezekana kufanya mabadiliko, tutimize wajibu wetu.

No comments: