2/5/07

TUTAENDELEA NA UBISHI HUU HADI LINI?


UTANGULIZI
Katika kukabiliana na ukweli, wanasayansi wa mazingira pamoja na watafiti wengine wameungana na sehemu nyingine ya jamii katika kuthibitisha kuwa mabadiliko yasiyo ya kawaida ya hali ya hewa ikiwemo ongezeko la joto duniani husababishwa kwa asilimia tisini na kazi za binadamu katika kujitafutia riziki. Asilimia kumi inayobaki inatokana na mabadiliko ya kawaida ya mwenendo wa dunia kama vile matetemeko ya ardhi na volkano. Ripoti ya tafiti za wanasayansi hawa kutoka maeneo mbali mbali hapa duniani imetolewa mwezi huu wa pili 2007. Ni kwa mara ya kwanza katika historia ya utawala wake, mwaka huu ambapo rais wa Marekani alitaja suala la uchafuzi wa hali ya hewa, napo alitamka kwa sekunde chache sana suala hilo hata bila kugusia undani wa tatizo lenyewe na wala hakufafanua atakavyofanya kukabili kadhia hiyo.


HALI HALISI
Kitakwimu nchi zilizoendelea ndio zinaongoza kwa kuchafua hali ya hewa, kutokana na moshi toka viwandani, zikiongozwa na Marekani. Kwa mujibu wa kitengo cha nishati cha serikali ya Marekani, takwimu zinaonyesha kuwa, hadi mwaka 1999, Amerika ya kaskazini (Marekani na Kanada) ndio walikuwa vinara wa kuchafua anga kwa hewa ya kaboni, kwa kiwango cha meta za ujazo milioni 1,720.4! Waliofuatia kwa uchafuzi ni nchi za Ulaya Magharibi, kwa kiwango cha meta za ujazo milioni 988.9. Viwango vya uchafuzi kwa maeneo mengine katika mabano ni Ulaya Mashariki (851.8), China (821.8), Asia (ukiondoa China na Japan, 700.8), Japan (296.7), Amerika Kusini (234.7), Mashariki ya kati (252.1) na Afrika (213.8). Takwimu hizi ni hadi mwaka 1999, na kwa sasa inaonyesha kwamba Marekani ndio inaongoza kwa uchafuzi ikifuatiwa na China. Pamoja na ukweli huu, inasikitisha kuona kuwa Wachina na Wamarekani ni kati ya watu wa mwisho kujadili athari za ongezeko la joto duniani, kwa sababu kuu kwamba iwapo watatakiwa kupunguza hewa chafu angani, basi viwanda vyao vingi vitadhoofika na hatimaye uchumi wao utayumba.

KILIO CHA DUNIA
Kutokana na mabadiliko haya ya hali ya hewa, kumekuwa na makongamano na mikutano kadhaa ya kimataifa katika kutafuta suluhu ya kudumu ya uchafuzi wa anga, kama nilivyowahi kuongelea katika makala zilizopita. Mojawapo ya mikutano hiyo ni ule uliofanyika katika mji wa Davos nchini Uswisi mwezi huu Februari. Mataifa makubwa yalikuwa yanajadili kuhusu biashara na suala la uchafuzi wa hali ya hewa likaibuka hapo. Katika mkutano huo pia, dunia ilimshangaa mkuu wa kampuni ya Nestle inayotengeneza vyakula, Bw Peter Brabeck-Letmathe aliposema kuwa suala la ongezeko la joto halina uzito wowote kwa sasa! Pia wakamshangaa mpinzani wa Bush kisiasa, Bw Al gore katika filamu yake ambapo anapinga suala la ongezeko la joto. Al Gore yeye anasema kuwa pesa zinazotumika sasa katika kukabiliana na ongezeko la joto duniani kupitia makubaliano ya Kyoto (ambapo Marekani haijatia saini) zingetumika katika kuboresha mindombinu ya maji pahala mbali mbali! huyu alikuwa mgombea uraisi ambaye alishindwa na Bush mnamo mwaka 2000.
Sina uhakika kama hawa watu walimaanisha kile ambacho waliongea ama walikuwa wanatania, lakini kwa sababu ni wafanyabishara nadhani walimaanisha kuwa hawana mpango kabisa wa kukabili tatizo hili la ongezeko la joto. Sasa mimi ninauliza, ubishi huu tutaendelea nao hadi lini?
Unaweza kusoma habari zaidi a mkutano huo hapa, hapa na hapa.

2/3/07

GARI LA MIONZI YA JUA HILI HAPA!


UTANGULIZI

Kumekuwa na usemi kwamba *Tembea uone*. Usemi huu una maana kubwa, kwamba ukiwa mtembezi basi utaona mengi. Pia kuna usemi unaoambatana na huo, kwamba Mtembea bure si mkaa bure, huenda akaokota! Basi katika pita pita yangu hapa na pale, kwa maana ya kwamba nilikutana na habari njema kwa watu wanaojali matumizi endelevu ya nishati na upunguzaji wa hewa chafu duniani. Nilikuta gari moja zuri katika makumbusho, ambalo kwa mujibu wa watu niliowakuta hapo wanasema kuwa lilikuwa linaendeshwa kwa kutumia umeme wa mionzi ya jua. Sababu za kwa nini kwa sasa halitembei ni kwamba hali ya hewa si nzuri sana kuweza kuchaji betri za umeme wa mionzi ya jua kwa mahali hapo, huwa mionzi ya jua si ya kutosha kuchaji betri hadi kuwa na ujazo unaotakiwa.


GARI LENYEWE

Katika boneti la mbele kwa juu kuna moduli kadhaa za kufyonza mionzi ya jua na kuihifadhi katika betri zake sita ambazo huwa zinafunikwa na boneti (sehemu ambayo huwa na radieta, kwa magari yanayotumia mafuta). Betri hizi zimeunganishwa pamoja na kutengeneza umeme mkubwa. Umeme huu hutumika kuendesha mota ambazo ndio husababisha nishati ya mwendo ili gari hili liweze kwenda. Kwa upande wa nyuma, katika buti pia kuna moduli kadhaa ambazo hufanya kazi kama zile za mbele. Gari hili huweza kuendeshwa muda wa masaa sita bila betri kupungua nguvu, kwa wastani wa mwendo wa kilometa arobaini mpaka sitini kwa saa, kwa mujibu wa maelezo ya wataalamu wa makumbusho hayo.


Binafsi nilifurahi sana kuweza kuona gari la ukubwa ule linaloendeshwa kwa kutumia mionzi ya jua, kwa sababu teknolojia hii ya kutumia mionzi ya jua kwa kuendesha mitambo si maarufu sana hapa duniani. Pia kuna magari madogo madogo mengi katika nchi zilizoendelea ambayo huendeshwa kwa kutumia betri za magari na mota, ambapo hayatumii mafuta, mara nyingi magari haya hutumiwa na walemavu wa miguu.



Katika ulimwengu huu kwa sasa ambapo tunajadili ongezeko la joto duniani, ni bora tukafikiri kutumia magari ya namna hii kwa safari ambazo ni fupi fupi, ili kupunguza kiwango cha hewa chafu ambayo husababishwa na uchomaji wa mafuta katika mitambo mbali mbali.
Tufikirie dunia mbadala.