9/20/06

YAJUE MALENGO YA MAENDELEO YA MILENIA

UTANGULIZI
Ni mara nyingi tumesikia, ama kuambiwa kuwa kuna malengo ya milenia, lakini huenda si wengi wetu tunaoyafahamu malengo hayo. Ni malengo yaliyoafikiwa mnamo Septemba 8 mwaka 2000, jijini New York Marekani na kuazimia kuwa ifikapo mwaka 2015, basi hayo maazimio waliyopanga yawe yametekelezwa kwa kiasi fulani cha kuridhisha, kama si kuyatekeleza kabisa.
Kwa ujumla kuna malengo manane ambapo nitayaeleza yote kwa ufupi katika makala hii na kuelezea lengo namba saba katika makala yake ya kujitegemea. Nitafanya hivi kwa sababu si busara kuelezea lengo namba saba pekee wakati malengo mengine hayafahamiki. Vile vile ni kwamba kufanikiwa kwa lengo moja basi ni njia ya mafanikio ya kuyafikia malengo mengine pia. Malengo haya yamewekewa viashiria, kujua kama yanatekelezeka ama la! Tafsiri kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili ni yangu!

YAFUATAYO NI MALENGO YA MAENDELEO YA MILENIA
1. Kupunguza Umasikini Uliokithiri pamoja na Njaa
Ndani ya lengo hili kuna malengo madogo mawili. Kwanza ni kupunguza hadi kufikia nusu, kwa kwa idadi ya watu ambao wanaishi kwa chini ya kiwango cha dola moja kwa siku, kati ya mwaka 1990 na 2015. (Kwa wakati huu, dola moja ya Kimarekani ni karibu sawa na shilingi 1200 za Kitanzania). Pili, ni kupunguza kwa zaidi ya nusu kwa idadi ya watu wasio na chakula.

2. Elimu Ya Msingi Kwa Wote
Kuhakikisha kuwa hadi mwaka 2015 mahali popote pale, watoto, kwa maana ya wasichana kwa wavulana wawe na uwezo wa kuhitimu elimu ya msingi.

3. Kukuza Usawa wa Kijinsia na Kuwawezesha Wanawake
Lengo ni kuondoa tofauti za kijinsia katika shule za msingi na sekondari hadi mwaka 2005 na katika nyanja zote kabla ya mwaka 2015.

4. Kupunguza Vifo Vya Watoto Wachanga
Lengo ni kupunguza kwa theluthi mbili, idadi ya vifo vya watoto walio katika umri wa hadi miaka mitano, kati ya mwaka 1990 na 2015.

5. Kuboresha Afya za Akina Mama
Lengo ni kupunguza kwa hadi robo tatu, idadi ya vifo vya wanawake wazazi, kati ya mwaka 1990 na 2015.

6. Kukabili Virusi Vya Ukimwi/Ukimwi na Magonjwa Mengine Makuu
Lengo la kwanza ni kupunguza na kuukabili Ukimwi na kubadili mwelekeo wake ifikapo mwaka 2015. Lengo la pili ni ni kukabili na kutokomeza malaria na magonjwa mengine makuu hadi kufikia mwaka 2015.

7. Kujihakikishia Uendelevu wa Mazingira
Hapa kuna malengo matatu madogo. Lengo la kwanza hapa ni kuingiza misingi ya maendeleo andelevu katika sera na mipango ya mataifa mbali mbali na kubadili mwelekeo na upotevu wa rasilimali. Lengo la pili ni kupunguza hadi nusu kwa idadi ya watu wasio na maji safi ya kunywa na huduma za maji taka. Lengo la tatu ni kuboresha makazi ya watu angalau milioni mia moja hadi kufikia mwaka 2020.

8. Kuanzisha Ushirikiano wa Kimaendeleo Duniani
Hapa kuna malengo mawili madogo. Kwanza, ni kujenga misingi ya utawala wa sheria na inayotabirika na isiyo na ubaguzi katika mifumo ya biashara na fedha. (Hii inahusisha pia kujifunga na misingi ya utawala bora, maendeleo na kupunguza umasikini, kitaifa na kimataifa). Pili, ni kuyapa kipaumbele mahitaji ya nchi masikini sana duniani (hii inahusisha kuondoa vikwazo katika masoko huru na usafirishaji wa bidhaa nje ya nchi. Pia kupunguza (ama kuondoa kabisa) madeni ya nchi hizi masikini na kutoa misaada kwa nchi ambazo zinaonyesha mwelekeo wa kuondoa umasikini).
Unaweza Kuyasoma zaidi Malengo hayo Hapa

Kwa hiyo ndugu msomaji wa makal hii, haya ndio malengo ya milenia yaliyoazimiwa mwaka 2000.
Katika makala ijayo, nitawaleteeni mjadala wa kiundani wa malengo kadhaa, tukianzia na lengo namba saba.

9/8/06

KIJANI, NJANO NA MAZINGIRA!

UTANGULIZI
Ndugu wasomaji wa blogu hii, leo naleta kwenu wazo jipya ama mjadala mpya. Kama kawaida yetu, ni jadi kuwa mtu akitoa wazo basi nasi tunapata wasaa wa kuchangia mawazo yetu, aidha kwa kuboresha ama kukosoa. Kwa hiyo basi, kwa leo nitaongelea rangi za kijani na njano, ambazo kwa siasa za nchi yetu si rangi ngeni hata kidogo, lakini leo ni siasa za kijani na njano katika upande wa mazingira.

MADA
Kwa wakereketwa wa siasa za nchi yetu, kijani na njano ni rangi za bendera ya chama tawala na pia ni mbili kati ya rangi nne za bendera ya taifa letu. Kwa ujumla rangi hizi kwa bendera zote mbili huwakilisha utajiri wa maliasili vikiwemo mimea, wanyama na madini yapatikanayo nchini mwetu. Huo ndio ufafanuzi uliowekwa yakini na serikali na chama kwa bendera hizo. Kwangu mimi, rangi hizi ni zaidi ya hapo, na humaanisha mambo mengine pia. Kwa wanachama wa chama tawala, wao huadhimisha kuzaliwa kwa chama chao kila mwaka tarehe tano mwezi wa pili. Aghalabu sherehe hizi huwa na shamra shamra nyingi zikiambatana na upokezi wa wanachama wapya na uzinduzi wa matawi mapya ya chama. Kwa mujibu wa takwimu rasmi, chama tawala nchini mwetu kina idadi ya wanachama rasmi wasiopungua milioni tano, nje ya mashabiki. Si haba, kwa nchi ya vyama zaidi ya kumi vya siasa na watu milioni thelathini na tano.
Kwa maana hiyo basi, nafikiri katika shamra shamra hizi wanachama hawa hupata wasaa wa kubadilishana mawazo na kuelimishana. Ni bora pia wakaelimishana maana ya rangi za bendera za chama chao kama hawajaelezwa, hasa kwa wanachama wapya. Pia, ni bora wakaelimishwa matumizi sahihi ya rangi hizo.

WAZO
Iwapo kila mwaka katika tarehe tajwa hapo juu wanachama wangekumbushwa (au kuelimishwa?) namna ya kutunza ukijani popote pale walipo, basi katika suala zima la mazingira tungekuwa mbali sana. Hebu chukua mfano, kila mwanachama kati ya hawa milioni tano (acha mashabiki) alazimike kupanda miti miwili tu mahali panapostahili, katika kumaanisha ukijani wa bendera ya chama chake, basi kwa mwaka tunakuwa na miti milioni kumi! Si suala dogo wala porojo, na hii ni kwa siku moja tu kwa mwaka mzima. Ukichanganya na miti tunayopanda kila Januari, basi tungekuwa tunasikia kwa mbali sana suala la ukame na kukauka kwa vyanzo vya maji.
Lakini, hata si kwa kupanda miti, basi iwe ni kuokota taka na kuzihifadhi mahali panapostahili ili kutunza ukijani, nadhani bustani nyingi sana mijini zingekuwa kijani sana hadi sasa, badala ya kuzungushia uzio kila mahali penye bustani ili watu wasikanyage bustani zetu. Ni suala la elimu na utashi tu.

Kwani haiwezekani?
Jadili