6/13/06

UNG'OAJI WA MIANZI MKOANI IRINGA: NI SAHIHI?



UTANGULIZI
Ndugu wanablogu wenzangu, nimesoma makala ya Bw Johnson Mbwambo ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari za mazingira Tanzania, ambayo ilitoka katika gazeti la Nipashe tarehe saba mwezi Juni. Ilinivutia na kunishitua kidogo, lakini nikaona niisome na kutoa maoni yangu kuhusu utaratibu mzima wa Serikali ya Mkoa wa Iringa kuhusu mpango wa kung'oa mianzi katika vyanzo vya maji. Yeye Bw Mbwambo ameandika makala kutokana na mahojiano aliyofanya na viongozi wa Mkoa wa Iringa juu ya uamuzi wa serikali na NGO katika mkoa wa Iringa, wa kutaka mimea jamii ya mianzi iliyo katika vyanzo vya maji ing'olewe, kwa kuwa si rafiki wa mazingira, kwa maana ya kwamba inakausha vyanzo vya maji. Ningependa kuongelea masuala machache muhimu katika makala yake hiyo isemayo "Operesheni ya kung'oa mianzi yapamba moto mkoani Iringa" .

MIANZI NI NINI?
Hii ni jamii ya mimea ambayo wataalamu wa elimu-mimea wameiweka katika kundi la majani yanayotoa maua, na si miti. Hii inatokana na jamii nyingi za mianzi kuwa na sifa za majani zaidi kuliko miti. Mianzi hupatikana duniani kote, lakini hutofautina kutokana na tofauti ya hali ya hewa ya sehemu mbali mbali. Mianzi ya kitropiki ni tofauti na ile ya nchi za baridi, hivyo hivyo mianzi ya sehemu kame ni tofauti na mianzi ya sehemu zenye unyevu wa kutosha. Mimea hii hupatikana katika jamii ya Bambuseae. kuna jamii 91 na aina zaidi ya elfu moja za mianzi kote duniani na kila aina ina sifa tofauti kulingana na mahali aina hiyo ilipo.Jamii za mianzi hutofautiana kwa urefu, kuna ile ambayo ikikua sana hufikia sentimeta chache hadi kukomaa, na ile ambayo hukua hadi kufikia urefu wa meta arobaini hadi kukomaa. Upana wa shina la muanzi hupishana sana kati ya jamii na jamii kutoka milimita moja hadi thelathini. Hata utoaji wa maua wa mianzi hutofautiana sana. Kuna jamii ambazo hutoa maua baada ya miaka 28 tu na ile ambayo hutoa maua baada ya miaka 120, (rejea Troup 1921) Synchronous'Gregarious' Flowering Species Table. Kuna jamii nyingi za mianzi ambazo hukua kwa wastani wa sentimeta 30 kwa siku (futi moja!), na baadhi ya jamii nyingine zimewekwa katika rekodi kwa kukua kwa wastani wa sentimeta 100 (mita moja!)kwa siku.
Kwa hapa Tanzania, mianzi hupatikana katika mikoa mingi sana,kama vile Tanga, Mbeya, Iringa, Ruvuma na Rukwa na kadhalika na matumizi yake pia hutofautiana kati ya mkoa na mkoa.


MATUMIZI YA MIANZI
Aina za matumizi hutofautiana kati ya sehemu na sehemu, na kati ya jamii moja na nyingine. Kwa wenzetu Wachina mianzi michanga huliwa na ile iliyokomaa hutumika kutengenezea karatasi, na vile vile hutumika katika matambiko yao kwa kuombea umri mrefu wa kuishi. Kwa Wahindi, mianzi ni alama ya urafiki wa heshima, kwa maana kwamba mtu kukirimiwa kwa bidhaa za mianzi (kama viti, vikombe nk) humaanisha urafiki. Mianzi hutumika kutengezea vyombo vya ndani, kama vile vikombe, nyungo, vikapu na matenga. Kwa Wanyakyusa na Wasafwa wa mkoani Mbeya, kuna vifaa vya kukamulia na kuhifadhia maziwa ambavyo huita 'kitana' au 'tana'.Mianzi hutumika kutengenezea viti, vitanda na meza, mianzi hutengeza madaraja, hujenga nyumba ambazo husilibwa kwa matope pamoja na vyoo. Mianzi hutumika kutengeneza mikongojo (fimbo za kutembelea) na bakora, hutumika kutengenezea mitumbwi pamoja na sakafu. Kuna jamii ambazo hutengeneza filimbi za mianzi (zipo katika mikoa ya Morogoro, Mbeya, Iringa na Rukwa). Mianzi hupandwa sehemu za makazi kama uzio.
Kwa ujumla kuna matumizi mengi mno ya mianzi, ambayo si rahisi kuyaeleza yote hapa.
Kibiolojia, mianzi ina faida yake pia. Husaidia kuzalisha hewa ya oksijeni, ambayo ni muhimu kwa maisha ya wanyama.

Mkoani Iringa mianzi ina matumizi ya aina yake. Kwanza mianzi michanga hutumika kutengenezea pombe maarufu ya 'Ulanzi' ambayo husafirishwa hadi mikoa jirani ya Ruvuma na Mbeya. Mianzi hii michanga hukatwa inapofikia kimo cha kuanzia futi mbili hadi nne na hapo huwekwa kifaa maalum chenye uwazi kwa juu kilichotengezwa kwa mwanzi pia. Kifaa hiki hugema utomvu wote toka katika mwanzi mchanga na kuuhifadhi> Utomvu huu baadaye huchachuka na kuwa pombe-ulanzi. Ni pombe maarufu sana makoani hapo. Pili, mkoa wa Iringa ni maarufu kwa ulimaji wa nyanya. Mianzi hutumika kutengenezea matenga ya kuhifadhia na kusafirishia nyanya kwenda sokoni.Tatu, mianzi hutumika kutengeneza mazizi ya mifugo, hasa maeneo ya vijijini, pia ni bidhaa muhimu sana ya ujenzi wa nyumba, hii ni sehemu zote, yaani mijini na vijijini.

MGONGANO WA MASLAHI
Amri ya serikali ya mkoa wa Iringa kwa upande fulani inaweza kuwa sahihi, hasa kama kuna ushahidi wa kutosha wa kuweza kutumika kuhalalisha uondoaji wa jamii hii ya mimea katika vyanzo vya maji. Sina uhakika kama amri hii inatekelezwa mkoani Iringa pekee au na maeneo mengine yenye mianzi katika vyanzo vya maji. Tukumbuke kuwa, miaka michache iliyopita kulikuwa na mjadala kuhusu miti jamii ya eucalyptus, kwamba ukuaji wake huhitaji maji mengi, hivyo jamii hii ya mimea ilikuwa hatari kwa vyanzo vya maji. Uondoaji wa miti hii ulileta migingano katika maeneo mengi ya nchi, hasa ikizingatiwa kuwa ni miti tegemeo kwa sekta nyingi sana, hasa viwanda. Miti hii (eucalyptus)ni nishati kuu katika mashamba na viwanda vya chai vilivyopo nchini, na pia ni tegemeo kwa TANESCO kwa kuwa hutengeneza nguzo za kusambazia umeme kwa kutumia miti hii. Miti hii ni nishati tegemeo katika kukausha tumbaku. Ni kwa sababu hizi na nyingine, ambazo zilifanya amri kwa watu, ya kuondoa miti hii iwe na malalamiko kutoka kila upande.
Ni ukweli kuwa mianzi mingi imepandwa katika sehemu zenye maji (ikiwa ni pamoja na vyanzo vya maji, kwa kuona kwangu mashamba mengi ya mianzi katika mikoa ya Iringa na Mbeya. Sijapata uhakika kama kweli mimea hii hukausha vyanzo vya maji, ndio sababu nasisitiza kuwa ni vizuri kukawa na ushahidi wa kutosha usio na mawaa kama vile machapisho ya kitaalamu, kabla ya 'kuisulubu' mimea hii muhimu. Kwa upande wa wadau ambao hutegemea sehemu ya mapato yao kutokana na mianzi(kama vile wagema na watengeneza matenga),inawezekana wakawa na mwitikio hasi, hasa kama hawajaelimishwa vya kutosha kuhusu athari za mianzi katika vyanzo vya maji. Hawa wataona moja kwa moja kuwa ajira yao inayoyoma.
Kwa upande wa serikali, wao ni watekelezaji wa sera zilizotungwa na bunge, ambazo aghalabu huwa za manufaa kwa jamii kwa ujumla. Hivyo basi, si ajabu kwa serikali kutekeleza sera ambayo inaonekana kuwa ina manufaa kwa wananchi wake. Kwa mtazamo huo, kama serikali imeona kuwa mianzi haifai kuwa katika vyanzo vya maji, basi haina budi kuiondoa mimea hiyo katika maeneo ya vyanzo vya maji ili kuwanusuru wananchi wake na baa la ukame (kama lililotokea miezi michache iliyopita).

UPANDAJI MITI MBADALA
Katika makala ya Bw Mbwambo, serikali imetaja na kupendekeza aina kadhaa za miti ambazo zitapandwa katika maeneo ya vyanzo vya maji na sehemu nyingine ambazo mianzi itaondolewa.Miti hiyo ni migunga, mizambarau na mivinje. Kuna jamii nyingine za miti ya asili ambazo zipo mkoani Iringa na zinafaa kupandwa katika vyanzo vya maji. Jamii hizi ni mikuyu (sycamore/fig tree) "ficus sycomorus", mivumo "ficus sur" ,albizia gummifera, mikoche "hyphaene compressa" na mingine mingi. Hii inafaa sana katika ulinzi wa vyanzo vya maji.

MUHIMU
Kama kweli serikali imepania kuondoa mianzi katika vyanzo vya maji, basi ni bora wananchi wakaelimishwa kuilinda miti mbadala, ili isije ikahujumiwa na wale walioondolewa mianzi yao, hili lipo na laweza kutokea.

Ndugu msomaji wa makala hii, ni nani yu sahihi katika suala hili? Ni serikali, au ni wananchi walioishi na mianzi hii kwa muda mrefu?
Jadili

3 comments:

Ndesanjo Macha said...

Asante kwa mjadala wako huu uliotokana na makala ya Mbwambo. Sauti yako katika uwanja wa blogu ni muhimu sana.

Rashid Mkwinda said...

Mie nadhani hii iwe changamoto kwa wanamazingira, kwani naamini mianzi ina faida na hasara zake, lakini hebu na basi na tuangalie faida zake na tuzianishe huku tukizioanisha na hasara zake kisha tutapata muafaka kama mianzi inatakiwa kung'olewa ama la.

Lakini kwa mtazamo wangu mianzi ni moja ya zao ambalo kwalo kuna baadhi ya watu hunufaika kiuchumi kwa kuuza kilevi kitokanacho na zao hilo.

Vilevile zao hilo hutumika katika baadhi ya miji na vijiji kwa kuezekea nyumba kadhalika mianzi hutumika katika kutengeneza samani za ndani ya nyumba.

Zablon said...

Wadau mimi nimefurahi kusoma makala. Nina swali, mianzi inaoteshwaje? Natamani kuilima