KARIBU KATIKA BLOGU HII. JISIKIE HURU KUCHANGIA MAWAZO YAKO, ILI KUIFANYA DUNIA IWE MAHALI PEMA PA KUISHI!
12/10/2011

Jiunge na Harakati za Siku ya Blogu Duniani

Siku ya Blogu ni ipi?

Utangulizi
Ni tukio ambalo linawakutanisha waandishi na wamiliki wa blogu duniani kujadili kuhusu mada moja ambayo huwa imechaguliwa na kisha kuweka mada hiyo katika blogu zao anuwai. Siku hii ni tarehe 15 Oktoba ya kila mwaka na imekuwa ikiadhimishwa tangu mwaka 2007. Matukio ya siku hii huratibiwa na mtandao uitwao ‘Blog Action Day’ (http://blogactionday.org) .

Mada za Siku ya Blogu
Kwa miaka ya nyuma, mada zilizowahi kujadiliwa ni umasikini (ufukara), maji na mabadiliko ya tabianchi. Mwaka jana 2010 mada iliyokuwa imechaguliwa ilihusu maji, kwa hiyo wanablogu duniani kote tulishiriki katika majadiliano kwa njia ya mtandao kuhusu suala la maji, kwa upana wake. Binafsi, nimeandika mada anuwai kuhusu maji na mazingi (kwa kuwa ndiyo taaluma yangu ilikoegemea). Mwaka huu, siku ya blogu duniani imesogezwa mbele kwa siku moja ili kushabihiana na siku ya chakula duniani (tarehe 16 Oktoba), kwa hiyo mada kuu ya mwaka huu inahusu CHAKULA! Kwa maana hiyo basi, wanablogu mbalimbali duniani wataandika mada mbali mbali kuhusu chakula, iwe ni upatikanaji wake, uhifadhi, uandaaji, matumizi, uharibifu, maadili katika usindikaji, ulafi, uhaba na namna tunavyowezesha upatikanaji wa chakula kwa jamii zote duniani na kadhalika.
Unakaribishwa kushiriki katika majadiliano haya, pia unaweza kujisajili katika mtanda wa Blog Action Day katika anuani niliyoiweka hapo juu!
Ahsante sana.

24/02/2011

Mgao wa Umeme, utaishaje?

Mgao wa umeme
Historia inaonesha kwamba mgao usio wa kawaida wa umeme kwa nchi yetu kwa miaka ya karibuni ulianza mwaka 1992, kufuatia ukame wa muda mrefu ambao uliikabili nchi kwa sehemu kubwa, ukizingatia kwamba kwa kipindi hicho, sehemu kubwa ya umeme uliokuwa ukitumika hapa nchini ilitokana na nguvu ya maji (hydropower) na mafuta mazito (Heavy Fuel Oil – HFO). Kwa kipindi hicho, umeme utokanao na gesi asilia ulikuwa bado haujaanza kuzalishwa kwa kuwa miundombinu ya uzalishaji na usafirishaji wa gesi ilikuwa haijajengwa.
Mahitaji makubwa ya umeme kwa sasa hayaendani kabisa na kasi ya uwekezaji katika miundombinu ya uzalishaji wa umeme, suala hili limesababisha kiwango kidogo cha umeme unaozalishwa kugawiwa kwa wateja wachache kwa muda fulani, hivyo kuleta kitu kinachoitwa mgao wa umeme. Kabla hatujaingia katika mjadala wa namna ya kuondokana na mgao, ni vema tukaangalia historia 'fupi' ya mgao wa umeme tulionao.
Nilichoandika hapa chini nimechukua kutoka katika vyanzo mbali mbali, ikiwemo katika machapisho ya shirika la Tanesco, makala za magazeti, makala za mtandaoni na mahojiano binafsi na watendaji wa shirika hilo na mahojiano na wadau mbalimbali wa sekta ya nishati.
**************************************************************************
Historia Kidogo
Kati ya mwaka 1996 na 2006 kilikuwa ni kipindi cha ubinafishaji wa mashirika ya umma kwa nchi yetu. Katika kipindi hiki mashirika mbali mbali ya umma yaibinafsishwa kwa wawekezaji mabepari ili kuyaendeleza. Katika orodha ya mashirika ya kubinafsishwa, Tanesco ilikuwemo. Ili kuiandaa Tanesco kubinafsishwa, serikali 'Haikuwekeza' rasilimali katika shirika hili, hivyo vitu vya msingi kama vile miundombinu ya uzalishaji umeme, usafirishaji na usambazaji, kuajiri nguvukazi mpya kila mara havikufanyika. Vitu hivi ni vya msingi sana katika suala zima la uhai wa shirika.
Ikumbukwe kuwa katika kipindi hicho, uchumi wa nchi ulikua kwa kiwango cha asilimia 7 kwa mwaka na kiwango hicho kiliendana na uwekezaji mkubwa katika migodi, kampuni za simu, kukua kwa sekta ya ujenzi (wa majengo ya kibiashara), kufunguliwa kwa mashamba makuwa yenye viwanda vya kusindika mazao, na kukua kwa sekta ndogo na za kati kiuchumi (small and medium sized enterprises). Sekta hizi ni watumiaji wakubwa wa umeme, hivyo waliongeza idadi ya wateja wakubwa wa umeme. Hadi kufikia mwaka 2002, shirika hili lilikuwa halijabinafsishwa, na kama nilivyotaja hapo awali hakukuwa na uwekezaji mkubwa tangu mwaka 1996.

Ujio wa Net Group Solutions
Mnamo mwaka 2002 serikali iliamua kuliweka shirika hili chini ya menejimenti kutoka nchini Afrika Kusini (Net Group Solutions) ili kukusanya mapato ya wadaiwa wakubwa na kuliandaa shirika na kubinafsishwa. Kampuni hii ilifanya kazi katika shirika hili hadi mwaka 2006 ya kukusanya madeni kutoka kwa wadaiwa wakubwa kama vile taasisi za serikali, jeshi, serikali ya Zanzibar na viwanda vikubwa. Ufanisi wa utendaji wa kampuni hii bado unatiliwa mashaka na wadau wengi, kwani haikusaidia kuondoa matatizo yaliyokuwa yakikabili shirika la umeme. Hatimaye mnamo mwaka 2006, serikali iliamua kutolibinafisha shirika lake. Mpaka hapo ikawa miaka 10 imeshapotea, ndani ya kigugumizi cha ugumu wa maamuzi ya 'Tubinafsishe' ama 'Tusibinafsishe'?.

Uwekezaji mpya kwenye umeme
Baada ya mwaka 2006 ndipo zikaanza juhudi za uwekezaji katika miundombinu ya umeme, mpaka sasa. Kwa mujibu wa ripoti ya mwezi Januari ya Tanesco, mahitaji ya umeme ni kiasi cha megawati 833, na mpaka mwezi huo shirika lililikuwa likizalisha kiasi cha megawati 1006 kutoka vyanzo mbali mbali kama vile maji, gesi na mafuta mazito. Katika kiwango hicho cha uzalishaji, umeme unaopatikana muda mwingi ni megawati 650 tu, hivyo hautoshelezi mahitaji. Ongezeko la mahitaji kila mwaka ni kati ya megawati 100 na 120. Hadi mwezi Juni mwaka 2011 ni megawati 145 tu ndizo ambazo zimeingizwa katika gridi ya taifa, hivyo suala la upungufu wa nishati hii bado ni kitendawili.

Hatua za dharura za uzalishaji umeme
Kimbilio kubwa la serikali katika kutatua janga la mgao imekuwa ni suluhisho la muda mfupi, la kutumia mitambo ya dharura ya kukodi ili kuzalisha umeme. Mitambo hii ambayo hutumia mafuta mazito na/au gesi na hutugharimu pesa nyingi kama taifa hivyo kuzorotesha uchumi. Hili ni pigo kwa uchumi wetu ambao bado ni mdogo. Suluhisho hili la muda mfupi la uhaba wa nishati haliwezi kutupeleka mbali, zaidi ya kutuongeezea umasikini. Kiwango cha gesi kinachopatikana sasa kwa ajili ya uzalishaji umeme ni kidogo, kwa sababu ya ufinyu wa miundombinu ya usafirishaji wa gesi kutoka mahali inapozalishwa kisiwani Songosongo hadi mahali inapotumika, Dar Es Salaam. Hivyo, hata kama mitambo ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi itanunuliwa na kufungwa leo, bado hatuwezi kupata umeme kwa sababu tuna upungufu wa gesi ya kuendeshea mitambo hiyo.


Tufanyeje kuepukana na mgao?


Utashi wa kisiasa
Kwa hili, kwa mtazamo wangu, kwanza kabisa kunahitajika utashi wa kisiasa (political will) wa wale tuliowakabidhi jukumu la kutuondolea umasikini. Utashi wa kisiasa ndio unaofanya kuwe na kigugumizi au maamuzi ya wapi tuweke rasilimali nyingi na wapi tuweke chache kulingana na vipaumbele vyetu vya taifa. Hatujawekeza rasilimali za kutosha katika utatuzi wa muda mrefu wa janga la upungufu wa nishati, hasa umeme. Kwa ulimwengu wa dijitali tulio nao, suala la upatikanaji toshelevu wa nishati linatakiwa kuwa ni kipaumbele namba moja. Huwezi kuongelea kilimo cha kisasa cha kuongeza thamani ya mazao kupitia usindikaji, iwapo huna umeme wa kuaminika. Huwezi kuongelea suala la kukuza sekta ya madini iwapo huna umeme wa kuaminika. Huwezi kukuza viwanda iwapo huna uhakika na umeme. Hakuna mwekezaji atakayekubali kupoteza rasilimali zake kwa kuwekeza mahali ambapo umeme si wa uhakika.

Uwekezaji mkubwa katika sekta ya nishati
Binafsi, sijaona mipango MADHUBUTI na INAYOTEKELEZEKA kwa rasilimali tulizonazo, ya kufanya uwekezaji mkubwa katika suala la nishati, hasa kwenye nishati jadidifu. Mpango wa serikali wa hadi mwaka 2015 ni kuzalisha megawati karibia 3000 na kuingiza katika mfumo wa gridi ya taifa. Mipango hii inategemea sana hisani ya wafadhili na mikopo. Binafsi sio mchumi, lakini natilia shaka sana mpango huu, kwa sababu kama taifa hatujaweka jitihada za kutosha kutoka vyanzo vya ndani vya mapato kugharamia miradi hii. Nimesoma bajeti za serikali kwa mwaka 2010/2011 na 2011/2012, bado hakuna mipango madhubuti ya uwekezaji mkubwa kutoka vyanzo vya ndani, kwenye nishati. Kwa miaka ya hivi karibuni, uchumi wa dunia umeyumba sana, na bado mpaka sasa katika nchi za Ulaya zinazotumia sarafu ya Euro uchumi haujatulia. Umoja wa Ulaya pamoja na serikali ya Marekani ndio wafadhili wakubwa wa miradi mingi ya nishati nchini kwa sasa, hivyo mtikisiko katika uchumi wao unaweza kubadili mwelekeo wa sera zao, kutoka kufadhili miradi na kutoa mikopo kwa nchi zinazoendelea na kupelekea kuinuana wao kwa wao kiuchumi, kama wanavyofanya kwa uchumi wa nchi ya Ugiriki unaoyumba. Hili linawezekana. Iwapo hili la kubadili sera litatokea, basi uwekezaji katika miradi ya nishati kwa hapa nchini utayumba na hivyo kuathiri utekelezaji wa mpango wa megawati 3000. Lisemwalo lipo!

Kudhibiti Upotevu na wizi wa umeme
Kwa mujibu wa takwimu za Tanesco kwa mwaka 2010, zilizochapwa katika ripoti iliyofadhiliwa na Benki ya Dunia (Electricity loss Reduction Study, June 2011) , upotevu wa umeme huligharimu shirika kiasi cha dola za Kimarekani milioni 72. Katika umeme wote unaozalishwa, asilimia 20 ya umeme wote haufiki kwa wateja (kwa mfano, kama zinazalishwa megawati 850, ina maana megawati 170 zinapotea kabla ya kufika kwa wateja). Hiki ni kiwango kikubwa sana cha upotevu. Katika upotevu huu, asilimia 25 inatokana na ubovu na/au uchakavu wa miundombinu na asilimia 75 inatokana na upotevu kwenye mauzo. Takwimu hizi zinasikitisha kwa sababu shida kubwa ya upotevu haiko kwenye miundombinu kama wengi tunavyotarajia, ila kwenye mauzo (udanganyifu na ukosefu wa uadilifu). Iwapo kuna utashi wa kisiasa, asilimia hizo 75 ambazo zinatokana na (mkono wa mtu) zinaweza kudhibitiwa kabisa. Hasara hiyo ya dola milioni 72 inaweza kudhibitiwa na kuongeza kipato katika bajeti ya taifa.

Udhibiti wa mikataba tata ya uzalishaji umeme
Kumekuwa na matatizo kwenye mikataba ya uzalishaji umeme inayosainiwa kati ya serikali na kampuni binafsi. Mikataba mingi imetokana na mpango wa dharura wa uzalishaji umeme, hasa kunapokuwa na shida ya mgao. Mikataba hii imetokana na maamuzi mabovu ya makusudi ya watendaji waliopewa dhamana ya kusaini mikataba hii kwa niaba yetu. Udhibiti wa mikataba mibovu unahitaji utashi wa kisiasa pia, kwa wale tuliowapa dhamana ya kudhibiti utendaji mbovu. Napendekeza kwamba kutungwe sheria (kama haipo), kwamba mikataba mikubwa, kama ile ya uchimbaji wa madini na uzalishaji mkubwa wa nishati, ipitie kwanza bungeni, na iwapo ina maslahi kwa nchi basi iidhinishwe na bunge kabla serikali haijatia saini kwa niaba yetu! Kwa mbinu hii, tutaweza kuwa na uzalishaji mkubwa wa umeme usio na mawaa, kwa kuwa kila kitu kitafanyika kwa uwazi kupitia wawakilishi wetu bungeni.

Hitimisho
Suala la umeme lina maslahi mapana kwa taifa, kiuchumi, kiusalama na kijamii, si la kulifanyia maamuzi ya mzaha na pupa. Uhaba wa umeme unaathiri uchumi wa nchi, kwani uzalishaji katika ofisi, mashamba na viwanda unategemea umeme. Mgao unaathiri sekta nyingine kama vile maji, ambayo husukuwa kwa pampu zitumiazo umeme, kutoka pale yanapotekwa kwenda pale yanapotumika. Tuchukue hatua madhubuti za kuepuka janga hili, kwa maendeleo ya taifa! Tutimize wajibu wetu!

Nimefungua mjadala, tuendelee kuelimishana.

02/02/2011

MKUTANO WA WALIOSOMA MALANGALI SEKONDARI - IRINGA

Kuna baadhi ya wenzetu waliona ni vema kuwa tuliosoma shule ya Sekondari ya Malangali tukutane mnamo tarehe 5/2/2011 saa tisa alasiri pale Chonya Bar Riverside, Ubungo Dar Es Salaam. Mfahamishe kila mmoja ambaye atakuwa na fursa.


Kwa mawasiliano:-


Faraja 0787 525 396


Mawazo Kibamba 0713 555 725




Karibuni sana



Picha: John Mwaipopo na mimi, tukifurahia jambo pembeni ya ukumbi wa mikutano wa shule, enzi tukisoma Malangali Sekondari. Picha hii ilipigwa mwaka 1997 .

20/05/2010

FAHAMU BAYOGESI

Utangulizi

Bayogesi (biogas) ni kitu gani?


Bayogesi ni mchanganyiko wa gesi inayoundwa na viasilia mbalimbali vinavyotengenezwa katika mazingira ya kutokuwepo hewa (oksijeni) ambayo asilimia kubwa ni gesi ya methane (CH4). Bayogesi ambayo aghalabu hutokana na kinyesi cha wanyama, masalia ya mimea na kinyesi cha binadamu inaweza kuzalishwa na kutumika kupikia na hata matumizi mengine kama vile kuendeshea mitambo mbalimbali. Matumizi ya gesi hii kwa mtu ambaye ana mifugo kama vile nguruwe, ng’ombe yanaweza kusaidia kuondokana na gharama za kununua nishati ya kuni, mkaa, umeme na hata gesi asilia inayochimbwa ardhini. Gesi hii inapunguza gharama za watumiaji wa vyanzo vingine vya nishati. Mfano, gharama za nishati ya umeme na gesi asilia ni ghali sana hasa kwa mtumiaji atakayedhamiria kutumia jiko la umeme au jiko la gesi lakini kwa gesi hii ya samadi mtumiaji itamgharimu muda wake tu kujaza samadi na maji kila siku na atakuwa hana malipo ya pesa kila mwezi kama itakavyomlazimu kulipia umeme na gesi asilia kila mwezi, na hata kuni ambazo watumiaji wengine hununua.


Mnyambulisho wa viambata Vya bayogesi


Kimsingi, bayogesi huwa na mchanganyiko wa gesi za aina mbalimbali, lakini inayopatikana kwa kiwango kikubwa ni gesi ya methane. Mgawanyiko huo kwa asilimia ni kama ifuatavyo:-


Methane (50%)


Carbondioxide (25%)


Naitrojeni (10%)


Sulphur dioxide ( 5%)


Haidrojeni (1%)


Gesi nyingine (9%)


Zingatia kwamba asilimia zilizooneshwa katika mabano zinaweza kubadilika kutokana na malighafi inayotumika kutengeneza bayogesi (samadi, majani, masalia ya chakula n.k.) na hali ya unyevunyevu wa malighafi hizo.


Uzalishaji wa bayogesi


Samadi ghafi inayotokana na kinyesi cha wanyama (kama vile kuku, nguruwe, ng’ombe na punda) kinaundwa na viasili vya Kaboni, Haidrojeni, Oksijeni Naitrojeni na Salfa. Viasili hivi hutengeneza sukari, mafuta na protini. Kinyesi au samadi humeng’enywa na bakteria ambao huvunjavunja kinyesi hicho kutoka katika hali ya protini, mafuta na sukari na kutengeneza muunganiko wa viasili ulio rahisi zaidi. Mmeng’enyo wa samadi (kinyesi) kwa kutokuwepo wa gesi ya oksijeni hutengeneza hewa ya ukaa (carbóndioxide). Mmengenyo wa samadi bila ya uwepo wa oksijeni huzalisha gesi ya methane (CH4) ambayo ndio inayowaka hasa. Gesi hii itokanayo na kinyesi huzalisha kilojuli 5,200 hadi 5,800 kwa meta moja ya ujazo.


Bayogesi huweza pia kuzalishwa kutokana na masalia ya mimea, kama vile masalia ya zao la mkonge, masalia ya kakao au masalia ya kahawa baada ya kutolewa ganda na nje. Malighafi hizi zote huweza kuzalisha bayogesi iwapo zitachachushwa katika mazingira yasiyo na hewa (anaerobic condition).


Aina za Mitambo ya Kuzalishia Bayogesi


Kuna aina kadhaa za mitambo ya kuzalishia bayogesi, ambayo inapatikana Tanzania. Aina hizi ni kama ifuatavyo.


Fixed Dome Biogas Digester (CAMARTEC/Hydraulic/Chinese)


Mitambo ya aina hii ilianza kutengenezwa nchini China kuanzia mwaka 1936 na ikasamabaa India mnamo mwaka 1937. Aina hii ya mitambo ya bayogesi hujengwa katika maumbo ya mviringo wa nusu duara, na huwa na sehemu kuu tano. Sehemu ya kwanza huwa ni sehemu ya kuchanganyia samadi na maji, sehemu ya pili ni ya kuchachushia, sehemu ya tatu huwa ya kuhifadhia gesi, sehemu ya nne ni ya kuhifadhia samadi ambayo imeshatumika kuzalisha gesi. Sehemu ya tano ni ile ya matumizi, yaani jiko au oveni, au jenereta.


Aina hii ya mitambo hujulikana sana kama CAMARTEC (kufuatia kusambazwa kwa wingi na kituo hiki cha kuhawilisha teknolojia za kilimo kwa ajili ya matumizi vijijini, kituo hiki kipo mkoani Arusha). Lakini pia, mpango wa serikali wa Miradi ya Gesi ya Samadi Dodoma (MIGESADO) ulijenga kwa wingi sana aina hii ya mitambo katika mkoa wa Dodoma. Shirika lingine linalohusika na ujenzi wa mitambo ya aina hii ni Shirika la Maendeleo na Uholanzi (SNV), lenye tawi lake mkoani Arusha. Nao wanajenga kwa wingi sana mitambo ya aina hii. Chanzo cha malighafi kwa mitambo hii ni samadi ya wanyama na kinyesi cha wanadamu.


Floating Drum/Gobar Biogas Digester


Aina hii ya mitambo sio maarufu sana kwa hapa kwetu Tanzania. Mitambo hii hutengenezwa kwa kutumia matanki makubwa ya plastiki (ya kuanzia ukubwa wa lita 1000), yanayobebana. Tanki kubwa huwa linatangulia chini na ndilo ambalo huwa na malighafi kwa ajili ya kutengenezea gesi. Tanki dogo hubebwa na hili kubwa, na huwa jepesi kwa sababu linakuwa linabeba gesi, kwa hiyo huwa linaelea juu ya hili kubwa. Tanki hili dogo huwa na kitu kizito cha kulikandamiza kwa juu yake, ili lisiweze kutumbishwa na upepo uvumao. Malighafi inayotumika kuzalishia gesi kwa mitambo ya aina hii ni masalia ya chakula yatokayo majumbani na mahotelini




< 3.Vacvina Biogas Digester


Asili ya mtambo huu ni nchini Vietnam, na inapatikana nchini Tanzania. Aina hii ya mitambo huwa na sehemu kuu nne ambazo ni tanki la kuchanganyia samadi na maji, tanki la kuchachushia samadi na kuzalishia gesi, tanki la kuhifadhia samadi iliyokwishatumia, mirija ya kusafirishia gesi kwenda katika vihifadhio, vihifdahio vya gesi (karatasi za nailoni ngumu) na sehemu ya kutumia gesi (jiko, oveni au jenereta). Matanki ya mtambo huu hujengwa kwa matofali ya kuchoma na saruji au matofali ya mchanga na saruji. Vitako vyaa matanki haya hujengwa kwa zege, ili kuongeza uimara na kuhimili uzito wa mchanganyiko wa samadi na maji.


Picha hiyo hapo juu inaonesha matanki ya kuchachushia masalia ya mkonge kwa ajili ya kuzalishia bayogesi, katika kiwanda cha mkonge kilicho Hale mkoani Tanga



4. Plastic Bag Biogas digester


Hii ni aina nyingine ya mitambo ya bayogesi ambayo inapatikana Tanzania. Uchachushaji wa malighafi kwa ajili ya kuzalisha gesi kwa kutumia mtambo huu hufanyika kwenye mfuko mgumu sana wa plastiki, ambao huwa na sehemu ya kuingizia mchanganyiko wa samadi na maji, na sehemu ya kutolea gesi kwwenda kwenye matumizi. Mfuko huu mgumu wa plastiki aghalabu hufukiwa ardhini ili kuulinda dhidi ya jua kali na kutoboka kutokana na shughuli za kibinadamu. Kwa aina hii ya mtambo, gesi huhifadhiwa katika sehemu ya juu ya mfuko huu, kabla haijasafirishwa kwenda kwenye matumizi. Mtambo huu ni wa gharama rahisi kidogo ukilinganisha na mingine ambayo imeorodheshwa hapo juu, kutokana na kutohitaji ujenzi unaohusisha matofali, zege ama saruji. Lakini shida yake ni kwamba mifuko hii haipatikani kwa urahisi hapa Tanzania, mara nyingi huagizwa kutoka nje ya nchi.




Picha: Vihifadhio vya bayogesi, kutoka katika mtambo wa Vacvina


Matumizi ya Bayogesi


Nishati katika Majiko


Bayogesi kutumika kama nishati katika majiko, kuendeshea mitambo kama vile magari na jenereta za kuzalishia umeme. Kwa Tanzania, bayogesi imekuwa ikitumika katika majiko maalum ya gesi kwa kupikia aghalabu na watu wenye mifugo ambao wana uhakika na upatikanaji wa samadi.



Picha: Majiko yanayotumia bayogesi


Nishati ya Kuendeshea Mitambo (mashine, magari, jenereta za kuzalishia umeme)


Bayogesi hutumika kuzalisha umeme. Mfano mzuri ni mtambo wa kuzalisha umeme ulio katika mashamba ya Katani Limited yaliyo katika mji wa Hale mkoani Tanga. Mahali hapo kuna jenereta ya ukubwa wa kilowati 150 kwa ajili ya kuzalisha umeme, ambayo huendeshwa kwa kutumia bayogesi. Kabla ya gesi kutumika katika mitambo, kwanza huchujwa kwanza katika chujio maalum lililo na kemikali za madini ya chuma, ili kuondoa gesi ya ‘hydrogen sulphide’ (H2S) ambayo huathiri sana mitambo kwa kusababisha kutu. Hali kadhalika, hewa ukaa (CO2) nayo huondolewa katika mfumo huu wa uchujaji huu, ili kufanya gesi ya methane iwe safi kabla ya kutumika katika mitambo husika. Kwa gesi inayotumika kuendeshea magari, yenyewe hupozwa kabisa na kuwa katika mfumo wa kimiminika, ili iwe rahisi kuhifadhiwa na kutumika. Magari ya namna hii yanapatikana nchini Sweden.




Picha: Jenereta ya kuzalisha umeme, inayoendeshwa kwa kutumia bayogesi. Ina ukubwa wa kilowati 150 na inapatika katika kiwanda cha mkonge cha Katani Limited, kichopo Hale Mkoani Tanga. Aliyesimama hapo kwenye jenereta ni Mhandisi Gilead Kissaka, meneja wa kiwanda .


Mbolea Itokanayo na Samadi Iliyokwishameng’enywa


Baada ya bayogesi kuzalishwa, masalia ya samadi ambayo huwa imemeng’enywa hutolewa nje ya tanki la kuchachushia mara samadi mpya inapowekwa katika tanki, kupitia chemba maalum ya kuingizia mchamganyiko wa samadi. Samadi iliyomeng’enywa hutumika kama mbolea ya kukuzia mimea. Inafaa sana kwa kustawisha mimea ya aina mbalimbali.










Kwa makala zaidi, bonyeza hapa na hapa


18/05/2010

NIMERUDI JAMVINI

Ndugu wanablogu wenzangu, majukumu ya kila siku ya kikazi yalikuwa yamenizidi mno, kiasi kwamba iliniwia vigumu kuweza kusoma na kuandaa makala za kujadiliana nayi hapa jamvini. Hata hivyo 'Ubize' haujaisha, ila umepungua kiasi, kwa hiyo nitajitahidi sana kuja na makala kadhaa za nishati na mazingira, ambazo ndio fani ninazojitahidi kubobea nazo kwa sasa.
Nimekuwa nikipita katika blogu zenu kujifunza hili na lile kila ninapopata nafasi na kuacha ujumbe kwamba nimepita. Lakini pia nafarijika kwamba baadhi ya makala na picha ninazobandika hapa zinatumika mahali pengine na huwa wanakumbuka kushukuru chanzo hiki, kwa hiyo ujumbe wetu huwa unafika mahali pengi zaidi na unasomwa.
Bila shaka tutaendelea kuwa pamoja kuendeleza mijadala kwa ajili ya maendeleo yetu.

Asanteni kwa uvumilivu!

Mwalyoyo

JINA: mwalyoyo
NILIPO: Dar Es Salaam, Tanzania
NILIVYO: Napenda kujadiliana na kubadilishana mawazo na wenzangu. Napenda kutoa na kupokea changamoto na fikra mpya, hasa zile ambazo zina lengo la kubadlisha maisha ya wanadamu kutoka hali moja ya kawaida kwenda hali nyingine nzuri zaidi. Ukiwa chanya na fikra zako zitakuwa chanya!Karibu tujadiliane.
ZAIDI  

YALIYOMO

MASKANI
MWONGOZO-JINSI YA KUBLOGU
NITUMIE UJUMBE

TOVUTI MSHABAHA

JET NA MAZINGIRA
BARAZA LA USIMAMIZI WA MAZINGIRA TANZANIA
UTUNZAJI MAZINGIRA NYANDA ZA JUU KUSINI
MKATABA WA KYOTO
MKATABA WA RIO
TAASISI YA NISHATI NA MAZINGIRA TANZANIA
EEDI TANZANIA
TFCG NA MISITU
WANASHERIA WA MAZINGIRA TANZANIA
BLOGU YA NISHATI MBADALA
MAENEO YA RAMSAR DUNIANI
MAENEO YA KIHISTORIA TANZANIA

KUHUSU BLOGU HII

Blogu hii ipo kwa ajili ya kuelimisha jamii kuhusu masuala mbali mbali ndani ya jamii hii pana, hasa masuala ya mazingira, nishati na maendeleo endelevu. Ingawa taarifa zilizo katika tovuti hii zinatolewa bure kwa ajili ya kuongeza uelewa katika jamii,si vibaya kama utataka kunakili ama kuzitumia, ila ni vyema na ni ustaarabu kama utataja kuwa umezitoa hapa. Asante

HIFADHI





 

BLOGU MBALI MBALI

JUMUIYA YA WANABLOGU TANZANIA
SAUTI YA BARAGUMU
MWANDANI
PAMBAZUKO
BINTI AFRIKA
KAZONTA
FATMA KARAMA
MRABA WA MAGGID
JARIDA LA UGHAIBUNI
KISIMA CHA WELEDI
MTANDAWAZI
MACHWEO
JITAMBUE
NGURUMO
FASIHI FASAHA
MOTO WAKA
FIKRA THABITI
MAWAZO HURU
KURUNZI
KASRI LA MWANAZUO
KITURURU
HARAKATI
DIRA YANGU
KISIMA CHA FIKRA
SAHARA SOUL FOOD
SWAHILI TIME
PILIKA VYUO VIKUU
UGOGONI
MTAFITI
WANAWAKE WA SHOKA
MAGGID MJENGWA
PICHA ZA MICHUZI
SAHARAN VIBE
FIKRA PEVU
MZEE WA MSHITU
MZEE WA SUMO

SOMA MAGAZETI

MAJIRA
NIPASHE
TANZANIA DAIMA
UHURU
DAILY NEWS
MWANANCHI
KIONGOZI
BUSINESS TIMES
THE CITIZEN
THIS DAY

MSANIFU: MWALYOYO


Idadi ya Waliopita Hapa

©MWALYOYO 2006. Haki zote zimehifadhiwa.